Skip to main content

AMOEBA NI UGONJWA WA TUMBO USIOFAHAMIKA KWA WATU WENGI

ugonjwa wa tumbo wa amoebaWatu wengi wanaugua magonjwa ya tumbo lakini ni wachache wanaofahamu kuhusu ugonjwa wa amoeba unaosababishwa na uchafu wa mazingira, vyombo vya nyumbani ambao huenezwa kupitia bakteria anayejulikana kama Entamoeba histolytica.
Vimelea vinavyoenezwa na bakteria huyu humsababishia mtu kuhara haja ambayo huonekana ina kamasi.
Ulaji wa matunda bila kuyaosha au kutokunawa mikono baada ya kutoka chooni, kula chakula bila kunawa mikono na kunywa maji yasiyochemshwa zinaelezwa kuwa ni baadhi ya namna zinazosaidia kuwasambaza bakteria hawa hivyo kuenea ugonjwa huu.
Mgonjwa hupata maambukizi baada ya kunywa au kula kitu kilichochanganyika na Entamoeba histolytica ambao hukimbilia kwenye utumbo mdogo ambako huzaliana.  Wakiwa wengi, huenda kwenye utumbo mkubwa na kuanza kushambulia mwili.
Wakikua, huishi katika kinyesi cha binadamu kisha hutolewa kwa njia ya haja kubwa na kuishi katika ardhi kwa muda wa wiki nne, kipindi ambacho huwa na uwezo wa kusababisha maambukizi kwa yeyote atayekutana nao.  Wanaweza kusambazwa kwa kutokunawa mikono vizuri baada ya kujisaidia, kusambazwa na nzi, kusafisha vyombo kwa maji yasiyo salama au kushikana mikono na mtu mwenye bakteria hao.
Kati ya watu milioni 40 mpaka 50 duniani kote wanasemwa kuugua ugonjwa huu ambao husababisha vifo 100,000 kila mwaka.  Mara nyingi, waathirika wengi huwa hawafahamu kama wanaugua maradhi haya hivyo kuchelewa kupata matibabu stahiki.
Walio kwenye hatari
Jamii inayoishi katika mazingira yasiyokuwa na maji salama ipo kwenye hatari ya kupata ugonjwa wa amoeba kwani huchota maji kutoka kwenye mito kwa matumizi ya nyumbani bila kujali kwamba hayakidhi vigezo vya kiafya.
Watu wasiosafisha vyombo vya chakula kwa maji salama au wanaotumia vyombo vilivyooshwa vikiwa bado vina majimaji wanajiweka kwenye hatari ya kupata maambukizi haya.  Vyombo vinatakiwa vifutwe kwa kitambaa safi mara tu baada ya kusafishwa.
Chakula kitakachochelewa kuliwa kinapaswa kufunikwa ili kuepusha inzi kutua kabla hakijatumika na kuacha bakteria wanaoneza maradhi haya.
Watu wengine wanaopaswa kuwa makini zaidi ni wale wasionawa mikono baada ya kutoka kujisaidia au wanaobanwa na haja sehemu ambazo hazina huduma ya choo na wanaotumia vyoo vya umma au wasafiri.
Dk Katoto Nestory kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) anasema wanafunzi na watu wanaokula kwenye vibanda vya mamalishe ambavyo havizingatii usafi wa vyombo vya chakula ni waathirika wakubwa wa ugonjwa wa amoeba.
Dalili
Mtu mwenye ugonjwa wa amoeba hukumbwa na dalili nyingi kama tumbo kujaa gesi, uchovu, kupoteza uzito, maumivu makali ya kichwa, kichefuchefu na kutapika.
Dalili nyingine ni homa, kutonusa vizuri harufu ya chakula na kutohisi ladha.  Wapo wagonjwa wanaopata maumivu makali ya tumbo, kunyonga na kupata choo kisichoisha (tenesmas).
Mgonjwa hupata choo kilichochanganyika na kamasi na endapo ataenda chooni mara nyingi huishiwa nguvu, wakati mwingine hushindwa kutembea.
Dk Katoto anasema mara nyingi watu huwa na bakteria wanaosababisha ugonjwa wa amoeba bila kuhisi dalili zake na kutahadharisha kwamba hata kuumwa tumbo au kuhara pekee hakutoshi kuthibitisha maradhi haya bali kupima choo ndio njia pekee ya kuthibitisha.
“Kuna watu ambao hawaumwi lakini wanao bakteria wanaosababisha ugonjwa wa amoeba miilini mwao.  Hawa ndio mara nyingi husababisha kuenea kwa ugonjwa huu kwani ingawa hawapati madhara huweza kuambukiza watu wengi,” anasema Dk Katoto
Madhara
Dk Katoto anasema ugonjwa huu unatakiwa kutibiwa mara tu mgonjwa anapogundulika na maambukizi ili kumuepusha na madhara mengi yanayoweza kujitokeza.
“Endapo mgonjwa hatapata matibabu kwa wakati anaweza kupungukiwa maji mwilini kutokana na kuharisha ambako kunaweza kusababisha kupoteza madini muhimu hivyo kuwa katika hatari ya kupoteza maisha, “ anasema Dk Katoto.
Madhara mengine yanayoweza kujitokeza endapo ugonjwa utachelewa kutibiwa ni kuhara damu kupindukia, kutapika, kusikia kizunguzungu, kukosa hamu ya kula na kupata homa kali.
Pia, mgonjwa atakuwa katika hatari ya kupata matatizo ya kujikunja kwa utumbo  endapo bakteria wanaoeneza ugonjwa huu watakuwa wengi.
Mgonjwa pia anaweza kupata vidonda kutokana na kutoboka kwa utumbo baada ya kushambuliwa na bakteria hawa ambao wanaweza kusafiri hadi kwenye ini na kumsababishia uvimbe.
Kujikinga
Ugonjwa huu, kwa mujibu wa wataalamu hutibika na kupona kabisa.  Inakadiriwa kwamba wiki mbili za matibabu kama mgonjwa husika amewahi matibabu zinatosha kumaliza tatizo hili.
Dk Katoto anasema mgonjwa anashauriwa kumaliza dozi atakayopewa ili kupona kabisa ndani ya muda aliopewa na daktari aliyemtibu.
“Kuna baadhi ya watu wana tabia ya kukatisha dozi pindi wanapohisi kupata nafuu.  Unapofanya hivyo unakuwa katika hatari ya kuumwa tena kwani ulipokuwa ukitumia dawa bakteria walidhoofika na unapoacha wanajijenga upya,” anasema Dk Katoto
Watu wanatakiwa kuchemsha maji ya kunywa ili kuweza kuua vijidudu vinavyosababisha ugonjwa, kuchimba vyoo, kunawa mikono baada ya kutoka chooni na kufunika chakula.
Unapoandaa chakula hakikisha unaosha matunda na mboga za majani kabla hazijaliwa.  Fanya hivyo kwa maji masafi, yanashauriwa yawe yanatiririka kama vile ya bomba au sinki la jikoni.
Unashauriwa kuepuka kula matunda na mboga isipokuwa uwe umeziandaa mwenyewe au una uhakika na aliyeziandaa.  Usinunue matunda yaliyomenywa na kuyala popote yanapouzwa.
Unapokuwa sehemu ya mbali na nyumbani hakikisha unakunywa maji au juisi za chupa pekee.  Usipende kutumia vinywaji hivyo kutoka vibandani au migahawa ambayo hauna uhakika na usafi wake.
Ukikosa maji ya chupa, hakikisha unachemsha maji ya kunywa au unayatibu kwa dawa zinazoshauriwa kama vile waterguard au iodine.  Haya ndio maji unayoshauriwa kuyatumia kuandaa juisi pia.
Usinywe maziwa yasiyosindikwa na bidhaa zozote zitokanayo kwani vyombo vinavyotumika kuandaa wanaweza wasizingatie kanuni zote za usafi.  Ikibidi yachemshe kabla hujayanywa ili kuwa na uhakika zaidi.
Epuka kula barafu na chakula kinachouzwa mitaani bila kuwa na uhakika wa maandalizi yake.  Kikubwa Zaidi, nawa mikono kwa sabuni kabla ya kula na kila baada ya kujisaidia.
Haufahamiki
Victoria Adolph, mkazi wa Mbagala Mtoni Kijichi anasema alikuwa haufahamu ugonjwa wa amoeba hadi mtoto wake alipougua na kulazwa hospitalini.
“Mwanzoni nilikuwa nampa dawa za kufunga kuharisha nikijua ni mchafuko wa tumbo lakini haikusaidia na alilazwa baada ya kupoteza maji mengi na kutundikiwa dripu tatu.  Hapo ndipo niliujua,” anasema Victoria.
Anasema madaktari walimshauri kuwahi kituo cha afya kwani ugonjwa huu hauna dawa za kutuliza maumivu kama ilivyo kwa maradhi mengine mfano maumivu ya kichwa.
Patrick Fundingoma, mkazi wa Tabata Relini anasema kukosa uelewa juu ya magonjwa kama amoeba kunaweza kusababisha kupoteza maisha kwa wasiopenda kwenda hospitali kwa wakati.
“Kuna baadhi ya watu hupenda kujihudumia kwa kumeza dawa bila kupata ushauri wa wataalamu wa afya jambo ambalo si zuri na linaweza kuhatarisha maisha ya mhusika,” anasema Fundingoma

Comments

Popular posts from this blog

Dr. William Samoei Ruto: muuza kuku ambaye sasa ni rais wa Kenya

Ruto ameweka historia kwa kuwa mgombea wa kwanza wa urais katika Jamhuri ya Kenya kushinda kura za urais katika jaribio la kwanza. Amekuwa naibu wa kwanza wa rais kushinda kiti cha urais katika Jamhuri ya Kenya. Mwanasiasa ambaye hajawahi kushindwa katika uchaguzi wowote. Mwanasiasa ambaye ametajwa na wachambuzi kama mchapa kazi na mwenye bidii na kiu ya kupata kile anacholenga maishani. Mtu asiyekata tamaa. Mcheshi katika hotuba zake, anayesemekana kutaka kujua kila linaloendelea karibu naye, mtu mkarimu mwenye roho ya kuchangisha pesa kwa watu na kwa ajili ya miradi mbalimbali. Ruto ameshutumiwa kwa kashfa kadhaa hasa za ufisadi bila kesi kufikishwa mahakamani, na ameshinda karibu kesi zote ambazo zimewahi kufunguliwa mahakamani dhidi yake ikiwemo kesi katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu ICC. Yafuatayo ndiyo mambo muhimu yanayomhusu rais wa 5 wa Jamhuri ya Kenya Dr. William Samoei Ruto. Majina Kamili: William Samoei Arap Ruto Umri: miaka 55 Mke wake: Rachel Chebet Ruto ...

Jioni

Download Audio The post Jioni appeared first on soka letu . source https://mjombazecoder.website/54168/

Bunge la Somalia limemchagua tena Rais wa zamani Hassan Sheikh Mohamud kuwa rais ajaye

Bunge la Somalia limemchagua tena Rais wa zamani Hassan Sheikh Mohamud kufuatia upigaji kura uliofanyika Jumapili mjini Mogadishu. Upigaji kura huo ulifanyika katika uwanja wa ndege wa Mogadishu uliokuwa na ulinzi mkali huku wanajeshi wa Umoja wa Afrika wakilinda hema la Afisyone ambalo lilikuwa ni sehemu ya kupigia kura. Katika kikao cha pamoja cha mabaraza mawili ya bunge yenye wajumbe 328 waliwapigia kura wagombea 36 wa urais katika duru tatu. Mohamud alimshinda Rais aliyekuwa madarakani Mohammed Abdullahi Mohamnmed maarufu kama “Farmaajo” katika duru tatu za upigaji kura. Hassan Sheikh Mohamud alikuwa rais kati ya Agosti 2012 na Februari 2017. The post Bunge la Somalia limemchagua tena Rais wa zamani Hassan Sheikh Mohamud kuwa rais ajaye appeared first on soka letu . Via soka letu https://ift.tt/ZmsWCwT