Iwapo itagundulika uwepo wa H. pylori tiba inayotumika ni kuchanganya dawa za antibayotic (antibiotic) za aina tofauti kama Amoxicillin, Tetracycline, Clarithromycin au Metronidazole na dawa zenye uwezo wa kupunguza uzalishaji wa tindikali kwa wingi au kwa kitaalamu Proton Pump Inhibitors (PPI). Wakati mwingine daktari anaweza pia kuongeza dawa ya Bismuth Compound.
Kwa wagonjwa sugu, dawa za antibiotic za aina tatu tofauti zinaweza kutumika. Dawa hizi ni pamoja na Amoxicillin + Clarithromycin + Metronidazole ambazo hutumika sambamba na dawa yeyote moja kutoka kundi la PPI kama vile Omeprazole au Pantoprazole pamoja na Bismuth Compound.
Kwa mgonjwa wa kawaida ambaye si sugu tiba bora inayoshauriwa ni kuchanganya dawa za antibiotic za aina mbili kama Amoxycillin + Metronidazole sambamba na dawa yeyote moja ya jamii ya PPI kama Pantoprazole.
Iwapo hakuna ushahidi wa kuwepo kwa uambukizi wa bakteria, dawa yeyote moja ya jamii ya PPI yaweza kutumika kwa muda mrefu zaidi bila kuchanganya na antibiotic yeyote.
Kwa kawaida kitendo cha kutibu na kuwaondoa Helicobacter Pylori humaliza na kuponyesha kabisa vidonda vya tumbo.
Hata hivyo, inawezekana kabisa ugonjwa huu kujirudia tena, hali ambayo hulazimisha kurudiwa tena kwa matibabu kwa kutumia aina nyingine ya antibiotics.
Aidha msomaji, unashauriwa si vyema kwa mgonjwa kujitibu mwenyewe bila kufuata ushauri wa daktari ili kuepuka madhara yanayoweza kutokea iwapo dawa hazitatumiwa inavyopaswa.
Ni kweli Maziwa ya ng’ombe yanaponyesha vidonda vya tumbo?
Kinyume na dhana iliyozoeleka ndani ya jamii, maziwa ya ng'ombe hayaponyeshi vidonda vya tumbo, bali huongeza madhara yatokanayo na ugonjwa huu. Hii ni kwa sababu, maziwa huwa na tabia ya kutengeneza aina fulani ya kinga au ukuta (protective coat) kwa vimelea vya Helicobacter Pylori ambayo huvikinga vimelea hivi dhidi ya mashambulizi ya dawa na hivyo kufanya dawa kushindwa kuwaua na kuwaondoa kabisa vimelea hivi.
Kinachotokea ni kuwa, maziwa huondoa tu kwa muda maumivu ya tumbo kwa kupunguza makali ya tindikali iliyopo tumboni. Pindi maziwa haya yanapoisha, maumivu hurejea tena na kuwa makali kama hapo awali.
Matibabu ya vidonda vya tumbo kwa njia ya upasuaji
Zipo aina nyingi ya upasuaji unaofanywa ili kutibu ugonjwa huu. Kuvuja damu ndani ya mwili kupitia vidonda vya tumbo ni sababu mojawapo ya kufanyiwa upasuaji kwa vile ni hatari sana hata kupelekea kifo iwapo mgonjwa hatapata tiba haraka
- Endoscopy: Ni njia inayotumika kutibu uvujaji wa damu unaotokana na vidonda vya tumbo. Aina hii ya tiba hutegemea sana aina na sehemu vilipo vidonda vya tumbo. Tiba hii yaweza kufanyika kwa kuchoma sehemu inayovuja damu ndani ya tumbo au utumbo kwa lengo la kusitisha uvujaji wa damu (cautery) au kwa kuvifunga vidonda kwa kutumia vifaa maalum (clippings). Aidha tiba hii ni nzuri na haina madhara yeyote yale.
- Madaktari wengi hupendelea upasuaji ujulikanao kitaalamu kama simple oversewing sambamba na tiba ya kuondoa bakteria. Aidha, mgonjwa pia hushauriwa kuacha matumizi ya dawa za NSAIDs kwa ajili ya kuondoa uwezekano wa damu kuendelea kutoka kwa vile kama ilivyoonekana hapo awali, matumizi ya dawa hizi huweza kusababisha uvujaji wa ndani kwa ndani ya mwili.
- Wagonjwa sugu, hufanyiwa baadhi ya upasuaji ambao huitaji utaalamu wa hali ya juu katika kuondoa neva na mishipa ya fahamu yenye kuhusika na uzalishaji wa tindikali katika tumbo.
Comments
Post a Comment